Alhamisi, 24 Oktoba 2013

TAZAMA SEHEMU YA HOTUBA YA ATHUMANI JUMANNE NYAMLANI MGOMBEA WA URAIS WA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA TFF



HOTUBA YA ATHUMANI JUMANNE NYAMLANI KWENYE MKUTANO WAKE NA WAANDISHI WA HABARI ALHAMIS TAREHE 24 OKTOBA 2013

Ndugu waandishi, Napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwenu nyinyi binafsi na vyombo vyenu vya habari kwani ni kweli kwamba mmeacha kazi nyingi na za muhimu na kunipa nafasi ya kuongea nanyi siku ya leo.
Nasema Ahasanteni sana.

Ndugu waandishi, Wito wangu kwenu hapa ni kutaka kuongea na watanzania wenzenu kupitia ninyi ambao kwa imani yangu nyinyi ndio kiunganishi kikubwa cha jamii. Napenda kuongelea kuhusu nia yangu niliyoionesha ya kugombea nafasi ya Rais wa shirikisho la mpira wa miguu Tanzania – TFF. Bila ya kuwapotezea muda naomba nianze kwa kukiri kwenu kuwa uamuzi wangu huu haukuwa rahisi kwasababu nafahamu majukumu mazito ambayo yanatakiwa kutekelezwa na Rais wa shirikisho la mpira wa miguu hasa kwa nchi kama yetu ambayo imekuwa ikikumbwa na changamoto mbalimbali katika uendelezaji wa michezo hasa wa soka.

Ndugu waandishi, wote wanafahamu kuwa nimekuwa kiongozi wa mpira wa miguu kwa muda mrefu sasa, katika ngazi mbalimbali kama inavyooneshwa katika kikaratasi changu chenye maelezo yangu mafupi nilichosambaza. Kwa hivi sasa ni makamu wa kwanza wa Rais wa shirikisho la mpira wa miguu nafasi ambayo nimekuwa nayo kwa takribani miaka  minne sasa nikiwa kama msaidizi mkuu wa mheshimiwa Leodger Chilla Tenga ambaye ni Rais wa shirikisho anayemaliza muda wake.

Ndugu waandishi, Ni kweli usiofichika kwamba katika kipindi cha uongozi wa mheshimiwa Tenga ambaye mimi nilikuwa msaidizi wake mkuu, tumepata mafanikio makubwa yakiwemo kujenga mfumo imara wa uendeshaji wa soka nchini kwa kuimarisha menejimenti ya soka, kuimarisha ligi kuu pamoja na ligi nyingine na kuimarisha timu za taifa. Mafanikio haya yaliongeza uaminifu wa shirikisho kwa wadhamini na wafadhili mbalimbali wa mashindano yetu nah ii yote ni kazi ya uongozi wa mheshimiwa Tenga.

Ndugu waandishi, Hakuna kazi yoyote inayoleta mafanikio bila kuwa na changamoto zake na nikiri kwamba tulikutana na changamoto mbalimbali katika utekelezaji wa majukumu yetu jambo ambalo kwa kiasi kikubwa ndilo lililonifanya niamue leo kufanya uamuzi huu mgumu kwa kuamua kuomba ridhaa ya watanzania kuongoza shirikisho hili kwasababu nazijua vyema changamoto hizi ambazo zimekuwa zikiukumba mchezo wa soka nchini na hivyo nitakuwa sijatenda haki kwa nafsi yangu, mchezo wa soka na taifa langu kwa kuwa mbinafsi kiasi hili cha kuamua kutogombea na hivyo kushindwa kutumia uzoefu wangu katika kuendeleza mafanikio tuliyoyapata na kutatua changamoto mbalimbali zilizojitokeza na zitakazojitokeza.

Ndugu waandishi, Sote tunafahamu kuwa ni hamu ya wapenzi na mashabiki wa soka nchini kuona kuwa tunapata mafanikio ya haraka katika soka hasa kwa kuzingatia uwekezaji tulioweka katika soka kwa kipindi cha takribani miaka nane sasa hasa suala la timu za taifa kushiriki katika mashindano ya kimataifa kama vile mashindano ya kombe la mataifa Afrika na kombe la Dunia jambo ambalo kwa maoni yangu na uzoefu wangu tunakaribia kulifikia na kama nitapata ridhaa ya watanzania (wajumbe wa mkutano mkuu) nitatekeleza mambo makuu tisa (9) ambayo ni:

1.      Kuimarisha usimamizi na menejiment ya soka katika ngazi zote
2.      Rushwa katika soka nchini
3.      Kukuza soka la watoto, vijana na wanawake
4.      Kuimarisha uwezo wa rasilimali fedha wa shirikisho
5.      Kuongeza idadi na ubora wa waamuzi, walimu wa soka na wataalamu wa Afya ya michezo
6.      Kuongeza ubora ligi kuu, ligi daraja la kwanza, ligi za wilaya na mikoa
7.      Kuongeza idadi ya mawakala wa wachezaji ambao ni watanzania
8.      Kuimarisha ushirikiano wa TFF na serikali
9.      Kuimarisha Ushirikiano wa TFF, CAF na FIFA.

Ndugu waandishi, Maeneo hayo tisa niliyokutajia hapo juu kwa ujumla wake kwa uzoefu wangu katika soka la Tanzania na Afrika yatasaidia kutatua changamoto mbalimbali tunazokumbana nazo mathalani ukuzaji wa soka la vijana kwaajili ya kuzalisha wachezaji wengi wenye uwezo wa kushindana na ambao wanaweza kukaa pamoja kwa muda mrefu.
Ndugu waandishi, Nawashukuru sana  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni