KATIBU Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban Ki Moon
ameueleza Mpango wa Afrika Kujitathmini Kiutawala Bora (APRM) kuwa nguzo muhimu
katika kukuza utawala bora barani humo.
Bw. Ki Moon pia amewapongeza viongozi wa nchi za
Afrika kwa kubuni na kutekeleza Mpango huo ambao ulianzishwa kutokana na mawazo
ya NEPAD katika kuhakikisha kuwa Bara la Afrika linakuwa na utawala bora ili
kuchagiza maendeleo.
Bw. Ki Moon alitoa pongezi hizi wiki hii jijini New
York alipokutana na viongozi waandamizi wa APRM na NEPAD ikiwa ni sehemu ya
kuadhimisha miaka 68 ya UN na Wiki ya Afrika na NEPAD.
Akizungumzia kuhusu APRM, Bw. Ki Moon alisema kwa
miaka 10 hii ya mwanzo tangu Mpango huo ulipoanzishwa, Bara la Afrika limeweza
kupiga hatua kwani mchakato huo unahimiza utawala bora, kuheshimu katiba na
kupanua demokrasia.
“APRM imeweza kusaidia kuweka utamaduni wa kisiasa
wa kuheshimu utawala bora miongoni mwa Serikali za Afrika. Mchakato huu umeweza
kuweka hadharani kanuni za kidemokrasia za kufuatwa na kuhimiza katika mijadala
kukabiliana na migogoro,” alisema.
Tanzania ni miongoni mwa nchi 33 kati ya 54 za Umoja
wa Afrika (AU) zilizojiunga na APRM na tayari imekamilisha Ripoti yake ya
kujitathmini inayoonesha hali ya utawala bora nchini.
Bw. Ki Moon alitumia wasaa huo pia kuzipongeza nchi
17 zilizokwishakamilisha Ripoti zao za kujitathmini. Tanzania na Zambia
zilitathminiwa Januari mwaka huu hivyo kufikisha idadi ya nchi hizo 17 kati ya
33.
“Nazipongeza nchi 17 zilizohitimisha tathmini
ya mwanzo. Mchakato huu umeweza kuimarisha uwajibikaji wa ndani ya nchi husika.
Katika baadhi ya maeneo APRM imeweza hata kuainisha viashiria vya migogoro na
kutoa mapendekezo juu ya namna ya kuitatua,” aliongeza.
Kutokana na thamani ya mchakato wa APRM, Bw. Ki Moon
licha ya kutaka Mpango huo uimarishwe zaidi, alizitaka nchi wahisani na jumuiya
ya kimataifa kuendelea kuupa msaada Mpango huo ili ufanikishe malengo yake.
Mwaka huu APRM imetimiza miaka 10.
“Miaka 10 iliyopita APRM ilianzishwa ikiwa ni
mchakato wa kijasiri ulioionesha dunia kuwa Afrika iko tayari kuchukua hatua za
kukabiliana na na changamoto mbalimbali inazokutana nazo katika ujenzi wa
demokrasia.
“Miaka kumi sasa, Mpango huu umethibitisha thamanai
yake. Katika kuadhimisha hili naziomba jumuiya za kimataifa kuzisaidia NEPAD na
APRM. Tuzisaidie kufikia hatua ambapo viongozi wa Afrika watakuwa wakizidi
kuwajibika kwa watu wao na kwa njia za kidemokrasia zaidi,” alisisitiza.
APRM ilianzishwa Machi 9, 2003 ikiwa na lengo la
kufanya tathmini za mara kwa mara za utawala bora miongoni mwa nchi wananchama
kwa lengo la kubaini changamoto za kufanyiwakazi na mambo mazuri ya kuimarishwa
au kuigwa na nchi nyingine.
Tanzania ilijiunga na Mpango huu mwaka 2004, Bunge likaridhia
APRM kuanza kazi nchini mwaka 2005. Januari mwaka huu Rais Jaakaya Kikwete
aliiwasilisha na kuitetea Ripoti ya Tanzania mbele ya Wakuu wenzake wa Nchi na
Serikali za APRM mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni