Alhamisi, 31 Oktoba 2013

MAPUNDA : SASA NARUDI NYUMBANI



 
Mlinda mlango wa mabingwa wapya wa ligi kuu soka ya nchini Kenya Gor Mahia Ivo Philip Mapunda,amesema kuwa kila kitu kinawezekana kwasasa baada ya kupata nafasi kurejea kwenye timu yake ya Taifa ya Tanzania bara baada ya kuwa nje kwa muda mrefu.
Kipa huyo kujumuishwa kwenye timu ya taifa ya Tanzania bara The Kilimanjaro Stars ambayo inajiandaa na michuano ya Chalenj itakayofanyika nchini Kenya kumezua mshangao mkubwa miongoni mwa mashabiki mbalimbali wa soka waliopo Kenya na Tanzania.
Mapunda ambaye ni mahiri kupangua mikwaju ya penalty amejumuishwa katika kikosi cha wachezaji 30 ambao watafanyiwa mchujo na kubakia wachezaji 10 watakaoungana na kikosi cha kwanza cha The Kilimanjaro Stars.
Mapunda amesema haijalishi yeye kuitwa kikosi cha kwanza au cha pili kikubwa ni kuonekana kwenye kikosi hicho ambacho kwa muda mrefu hajakitumikia na ameahidi kufanya jitihada zake kuhakikisha wanarejea na kikombe nyumbani Tanzania.
Michuano ya Chalenj inataraji kutimua vumbi kuanzia Novemba 27 hadi Disemba 12 mwaka huu na kipa huyo tegemezi wa Gor Mahia ataungana na makipa wengine akiwemo Aishi Manula kutoka Azam na Hussein Sharif kutoka Mtibwa katika kikosi kitakachofanyiwa na mchujo kabla ya kuungana na mlinda mlango namba moja wa Yanga Afrika Ally Mustapha Mtinge Barthez katika kikosi kamili kitakacho kwea pipa kuelekea Nairobi nchini Kenya.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni